KISUKARI INAUA TUZINGATIE USHAURI WA KITALAAM TUISHI
Na James Zakayo.
Kutokana na tafiti za
watalaam wanasema kisukari ni kundi la magonjwa yanayohusiana na ufanyaji kazi
wa mwili ambapo mtu anakuwa na kiwango kikubwa cha sukari aina ya glucose katika
mwili kutokana na mwili wako kukosa uwezo wa kutengeneza insulin ya kutosha au
seli za mwili wake haziwezi kutumia insulin iliyopo.
Mtalaamu wa tiba
lishe kutoka misungwi jijini Mwanza Amani Ezekiel kutoka Kliniki ya focus About tomorrow anasema kuwa
moja ya dalili kuu za ugonjwa huu wa kisukari ni hupata haja ndogo mara kwa
mara (polyuria), kusikia kiu kila wakati (polydipsia) na njaa (polyphagia).
“Kuna aina tatu za
kisukari; kisukari aina ya 1, kisukari aina ya 2 na kisukari aina ya 3,
Kisukari aina ya 1, mwili wa mgonjwa wa aina hii ya kisukari hautengenezi
insulin kabisa” anafafanua mtalaam.
Akiendelea kufafanua anasema mwili wa mgonjwa
wa kisukari wa aina ya hii mara nyingine huitwa insulin-dependent diabetes,
juvenile diabetes, au early-onset diabetes.
“Watu wa kisukari
aina hii wanapokuwa na umri wa chini ya
miaka 40 na hasa katika miaka ya mwanzo kabisa ya ujana wao. Kisukari cha aina
hii huwapata watu wachache ukilinganisha na aina nyingine za kisukari, karibu
asilimia 10 tu ya wagonjwa wote wa kisukari huwa na aina hii ya kisukari”
alisema Ezekiel.
Anasema mgonjwa
mwenye kisukari cha aina hii atapaswa kutumia sindano za kumwongezea insulin
mwilini katika maisha yake na lazima
kila wakati ahakikishe kuwa kiwango chake cha sukari mwilini kinakuwa sawa kwa
kuchukua vipimo na kufuata mpango wa chakula maalum.
Akiendelea kutoa maelezo anasema kuwa kisukari
aina ya pili, mwili hautengenezi insulin kwa kiwango cha kutosha au seli za
mwili zinashindwa kuitumia insulin iliyopo (insulin resistance). Karibu
asilimia 90 ya wagonjwa wa kisukari katika ulimwengu husumbuliwa na aina hii ya
kisukari.
“Watu
wenye unene usio wa kawaida na wenye uzito mkubwa wapo kwenye hatari kubwa
zaidi ya kupata kisukari cha aina hii ukilinganish na wale wenye miili ya
kawaida. Kuwa na uzito mkubwa au unene usio wa kwaida husababisha mwili kutoa
kemikali zinazovuruga mfumo wa namna ya mwili unavyotumia chakula
kilichoyeyushwa ili kuupa mwili nguvu na kuuwezesha kukua” alisema Ezekiel.
pia anaelezea kuwa na uzito mkubwa, kutofanya mazoezi na kutozingatia namna ya kula chakula kinachofaa, humweka mtu katika hatari kubwa ya kupata aina hii ya kisukari . “Kwa mfano, kunywa soda moja tu kwa siku kunaongeza uwezekano wa kupata aina hii ya kisukari kwa kiwango kikubwa sana”aliongezea mtalaam.
Ansema hatari
ya kupata kisukari cha aina hii huongezeka pia na umri, sababu kamili
haijajulikana bado lakini labda kwa vile umri ukiongezeka mtu huongezeka uzito
na hupunguza shughuli za kuutumia mwili wake.
Inaonekana pia kuwa
mtu mwenye ndugu wa karibu mwenye ugonjwa huu, naye pia huweza kuupata ugonjwa
huu. Watu wa asili ya Mashariki Ya Kati, Afrika na kusini mwa mwa Bara la Asia
hupatwa sana na kisukari aina ya pili.
Akifafanua anasema kuwa na kiwango kidogo cha homoni ya testosterone
kumeonyesha kuwa na mchango katika kusababisha aina hii ya kisukari.
Wataalamu wanasema
kuwa kuwa na kiwango kidogo cha testosterone katika mwili kunahusiana na tatizo
la mwili kutoweza kuitumia insulin (insulin resistance).
“Kuna baadhi ya watu
ambao wameweza kuudhibiti ugonjwa huu kwa kupunguza uzito wa miili yao, kufuata mipango mizuri ya
chakula , kufanya mazoezi ya miili yao na kuchukua vipimo vya mara kwa mara
kujua viwango vya sukari katika miili yao”aliongezea mtalaam.
Anasema lakini
kisukari cha aina hii ya pili ni ugonjwa unaokua kila siku na dalili zake
kuongezeka kila siku, hivyo mwishowe mgonjwa itabidi aongezewe insulin. Mara
nyingi wagonjwa wa aina hii ya kisukari mwishowe huongezewa insulin ya vidonge.
Akiendela kufafanua juu ya ugonjwa wa
kisukari anasema kisukari aina ya 3(Gestational
Diabetes) aina hii huwapapata wanawake
wakati wanapokuwa wajawazito.
“Baadhi ya wanawake
wanakuwa na viwango vikubwa sana vya glucose katika damu zao na miili yao haina
uwezo wa kutengeneza insulin ya kutosha kuweza kusafirisha glucose hiyo hadi
kwenye seli za miili yao hivyo kusababisha kuongezeka kwa kiwango cha sukari
katika miili yao”alisema mtalaam Ezekiel.
Anasema kuwa kisukari hiki huweza kudhibitiwa vizuri kwa kula chakula kinachofa na kufanya
mazoezi, ni asilimia ndogo kati yao ambao huhitaji kupewa dawa. Na isipodhibitiwa
huweza kusababisha matatizo wakati wa uzazi au kufanya mtoto anayezaliwa kuwa
mkubwa kuliko alivyostahili.
“Kisukari ni matokeo
ya matumizi ya baadhi ya vyakula na kushindwa kufanya kazi kwa baadhi ya
homoni, chakula baada ya kuyeyushwa huwa katioka mfumo wa glucose huingia
katika mfumo wa damu, seli za mwili hutumia glucose hiyo ili kupata nguvu na
kukua”anasema mtalaam.
Anasema kuwa lakini
seli haziwezi kuchukua glucose hiyo bila uwepo wa insulin, insulini ndiyo
inayoziwezesha seli hizo kuchukua glucose ukumbuke kuwa insulini hutengenezwa
na kongosho mwilini.
Pia anafafnua kuwa mtu
mwenye kisukari ni yule ambaye kiwango chake cha glucose katika damu ni kikubwa
mno (hyperglycemia) kutokana na kwamba mwili wake hautengenezi insulin ya kutosha
au seli kushindwa kuitumia insulin inayotengenezwa na kongosho.
Matokeo yake ni
kuongezeka kwa kiwango cha sukari katika damu ambayo baadaye hutolewa nje ya
mwili kupitia katika mkojo. Mgonjwa wa kisukari ana zahana kubwa ya glucose
katika damu yake lakini mwili unashindwa kuitumia glucose hiyo kwa matumizi
yake ili upate nguvu na kukua.
Mtalaamu huyo anashauri
kuwa ni watu wa kufanya mazoezi, kula vyakula vya asili na kuepukana na vyakula
vya viwandani kwa asilimia kubwa ikiwa ni pamoja na vyote vyenye sukari na kuwa
na mtindo wa kuangalia afya zetu kila mara kwani kisukari ni moja ya magonjwa
yanayomaliza idadi kubwa ya watu duniani.
Kwa takwimu za
shirika la afya duniani za mwaka 2015 zinaonesha kuwa takribani watu wapatao
milioni 38 hupoteza maisha kila mwaka kutokana na magonjwa yasio ya kuambukiza
ikiwemo kisukari.
Comments
Post a Comment